...

Washikadau Waungana Kupiga Vita Maambukizi Mapya Ya Virusi vya Ukimwi na mimba za mapema.

Dishon Amanya-Bungoma

Takwimu za hivi punde kutoka kwa Baraza la Kitaifa la Kudhibiti Magonjwa ya SDCC zimefichua kuwa vijana wenye umri kati ya miaka 13 na 35 sasa wanachangia asilimia 75 ya maambukizi mapya ya VVU.

Akizungumza wakati wa hafla ya uhamasishaji wa wanafunzi katika shule ya Sekondari ya Matili huko Kimilili, Douglas Bosire anayesimamia takwimu katika idara hiyo alisema mengi ya maambukizi mapya yanatokana na idadi kubwa ya unyanyasaji wa kijinsia dhidi ya vijana.

Kutoka Kulia: mwakilishi wa akina mama Bungoma Catherine wambilianga,seneta mteule Catherine Mumma

“Takwimu zinatia wasiwasi na kuna kitu kinahitajika kufanywa haraka ili kuokoa watoto wetu,” alisema.

Bosire anadokeza Kaunti ya Bungoma ilirekodi jumla ya mimba za utotoni 11,713 mwaka wa 2023, ikiwa ni asilimia 21, kile anachosema kimeimarika kidogo hadi 19%, hata hivyo, akisisitiza kuwa takwimu bado zinatia wasiwasi.

“Hii inarudisha nyuma maendeleo ya masomo yao kwani wengi wao hulazimika kuacha shule kwa muda au hata kabisa ili wawatunze watoto wao,” aliongeza.

Kongamano hilo la uhamasishaji lilihudhuriwa na seneta mteule Catherine Mumma ambaye amechukua hatua ya kuwaelimisha vijana dhidi ya tishio hilo la Triple Threat.

Mwakilishi wa akina mama Bungoma Catherine wambilianga

“Huu ni mpango ambao tumeuchukua kama viongozi ili kurejesha heshima ya vizazi vyetu vijavyo vilivyo hatarini kutoweka, watu wote wenye mawazo kama hayo wanapaswa kujitokeza kwa ajili ya watoto wetu wa kiume na wa kike,” alisema.

Aidha, anadokeza ni wakati muafaka kwa wasichana wadogo kuanza kupata Elimu ya Afya ya Uzazi ili waendelee kufahamu hatari zinazowakabili kujihusisha mapema katika shughuli za uzazi.

Nae Mwakilishi wa wanawake kaunti ya Bungoma Catherine Wambilianga alitumia fursa hiyo kuthibitisha kuwa wabunge katika Bunge la Kitaifa na Seneti wanafaa kutunga sheria zinazofaa ili serikali iweze kutoa  visodo  kwa shule zote ili kuhakikisha  wasichana wanaotoka katika familia zisizojiweza wananufaika.

Tishio hilo la Triple threat  linajumuisha maambukizi mapya ya VVU, Mimba za utotoni na Ukatili wa Kijinsia, jambo ambalo Baraza la Taifa la Kudhibiti Magonjwa limeahidi kupambana nalo kwa kuwahusisha washikadau mbalimbali.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Seraphinite AcceleratorOptimized by Seraphinite Accelerator
Turns on site high speed to be attractive for people and search engines.